Popular Posts

Saturday, 18 May 2013

POLISI WAZIDISHA NGONJERA KUUMIZWA KWA MWAANDISH WA HABARI (KIBANDA)



Jeshi la Polisi limekwepa kuwajibika kueleza kuhusiana na mchakato wa uchunguzi wa tukio la kutekwa, kupigwa, kuteswa na kujeruhiwa kwa Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Absalom Kibanda. Aprili mwaka huu Jeshi hilo liliahidi kwamba lingetoa taarifa kwa umma kuhusiana na uchunguzi wa timu iliyoundwa kuchunguza tukio hilo. Hata hivyo, maofisa waandamizi wameshindwa kutekeleza ahadi hiyo na kuunyima umma haki ya kujua waliotenda uhalifu huo wa kinyama na hatua zilizochukuliwa dhidi yao. Mara kadhaa, Msemaji wa Jeshi hilo, Advera Senso, na Naibu Mkurugenzi wa Upelelezi wa makosa ya Jinai (DCI), Isaya Mngulu, wamekuwa wakikwepa kulizungumzia suala hilo na kuahidi kuwa taarifa zitatolewa baadaye.

Kibanda ambaye pia ni Mhariri Mtendaji wa Kampuni ya New Habari (2006) Limited ambayo ni wachapishaji wa magazeti ya Rai, Dimba, Mtanzania, Bingwa na The African, alivamiwa na watu hao, wakati akirejea nyumbani kwake, Mbezi Juu, jijini Dar es Salaam Machi 5, mwaka huu. Jana NIPASHE iliwasiliana na Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai Nchini, Kamishna Robert Manumba, ambaye alisema hawezi kulizungumzia kwa kuwa hakuwapo wakati kikosi kazi kilipoundwa na kuelekeza aulizwe aliyekiunda. “Tume hiyo iliundwa lini?” alihoji na kuendelea: “Aulizwe aliyeunda atakuwa na majibu sahihi, mimi siwezi kueleza lolote.” Wakati kikosi hicho kinaundwa, DCI Manumba alikuwa nchini Afrika Kusini kwa ajili ya matibabu na Mngulu ndiye aliyekuwa anakainu nafasi yake.

No comments:

Post a Comment